Kigoma, Tanzania

Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kigoma imewakamata wahamiaji haramu 73, ambapo 56 wamethibitika kuwa wahamiaji haramu na 17 uchunguzi wa uraia wao unaendelea na wote hawa  wanashikiliwa  kwa kosa la kuingia nchini kinyume cha sheria.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari mapema wiki hii Kaimu Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kigoma Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji (ACI) Augustino Matheo amesema Idaa ya uhamiaji mkoa imefanikiwa kuwakamata wahamiaji haramu hao kutokana na kufanyika doria na misako mbalimbali iliyofanyika tarehe 03 Machi 2021.

ACI Matheo amefafanua zaidi kwamba waliokamatwa nia raia 51 wa nchi jirani ya Burundi, raia wa Kongo DRC 04, raia wa Rwanda 01 na Wanaodai ni raia wa Tanzania17 ambapo uchunguzi unaendelea ili kubaini uraia wao.

“Wahamiaji haramu hawa wamekamatwa katika mwalo wa ziwa Tanganyika eneo la Kibirizi mkoani Kigoma, Katika maelezo yao tumegundua walikuwa wanajishughulisha na uvuvi” alisema ACI Matheo

Aidha ametoa tahadhari kwa mwananchi yeyote atakayekutwa amewahifadhi wahamiaji haramu katika nyumba yake au akiwa anawasafirisha kwenye gari (chombo cha usafiri) atachukuliwa hatua kali za kisheria zikiwemo kushitakiwa mahakamani, nyumba au chombo alichokua anakitumia kusafirishia au kuwahifadhia wahamiaji haramu vinaweza kutaifishwa na Serikali kwa mujibu wa sheria.

Ameongeza kwamba tayari hatua zimechukuliwa mara baada ya kukamilisha  taratibu zote watafikishwa mahakamani ka kosa la kuingia nchini kinyume na sheria za nchi.

“Wale wote wanaoingia nchini kupitia vipenyo visivyo rasmi (Panya Roots) tutawakamata wote, vilevile tunawaomba wananchi watupe ushirikiano pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili tuwabaini wahamiaji haramu na mtandao wao” alisema

Onyo limetolewa kwa Mkoa wa Kigoma kwamba Mkoa huo sio kichaka wala njia au maficho ya wahamiaji haramu kupitia kwenda sehemu zingine za nchi, kwani Idara imejipanga kidete kuwezesha na kudhibiti uingiaji na utokaji wa watu kupitia utekelezaji wa sheria na kanuni zilizopo ili kulinda usalama wa Taifa na kukuza maendeleo ya kiuchumi.